WEMA VS DIAMOND WAONESHANA UBABE WA PESA

WAKATI 
Wema Isaac Sepetu akionesha jeuri ya fedha kwa kufungua bonge la ofisi ya kuzalisha filamu, zilipendwa wake, Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’ amemjibu kwa kukamilisha mjengo wa maana uliogharimu Sh. milioni 260 hivyo kwa pamoja kuthibisha msemo kuwa fedha inaongea, Ijumaa Wikienda lina data kamili.
Katika uzinduzi huo ambao Ijumaa Wikienda lilialikwa, Wema ndiye alikuwa wa kwanza kumshtua mama yake mzazi, Mariam Sepetu na mastaa mbalimbali (akiwamo Diamond), Jumatano iliyopita na kuzindua ofisi yake inayojulikana kwa jina la Endless Fame Films iliyopo Mwananyamala- Komakoma, jijini Dar.
Pamoja na mkali huyo ambaye ni sura ya mauzo kwenye gemu la filamu za Kibongo kumualika mama yake, ilibainika kuwa hakuwa amemtaarifu kabla kuhusu umiliki wa ofisi hiyo hivyo ilikuwa ‘sapraizi’ kwa mzazi huyo.
“Mama hii ndiyo ofisi yangu ambayo maandalizi yake yalianza tangu Juni, mwaka jana na sikutaka kukwambia hadi ilipokamilika ili iwe sapraizi,”  Wema alimwambia mama yake mbele ya wageni waalikwa na kuongeza:
“Nia na madhumuni ya ofisi hii ni kukuza vipaji vya wasanii wachanga hivyo nakaribisha chipukizi wa filamu waje kujiunga kwenye kampuni yangu.”
Bila kutaja gharama za ofisi hiyo, Wema alisema kwa kifupi kuwa imemgharimu mamilioni ya shilingi huku akiainisha vitu vilivyosheheni ndani kama jiko, ofisi yake, sehemu ya kunywea kahawa, kupumzikia wageni, vyumba viwili vya wahariri wa video pamoja na choo cha ndani.
Siku hiyo ilipambwa na mastaa mbalimbali wa filamu kwa ajili ya kumpa sapoti mwenzao (Wema) ambaye ameonesha kupiga hatua kubwa kwenye sanaa wakiongozwa na Vincent Kigosi ‘Ray’, Jacob Steven ‘JB’, Single Mtambalike ’Richie’, Issa Mussa ‘Cloud’, Hartman Mbilinyi na Husna Posh ‘Dotnata’.

Wakati mastaa waliofika kwenye sherehe hiyo ya Wema wakijiuliza juu ya kutohudhuria kwa Diamond,
taarifa zilizonaswa na gazeti hili zilidai kuwa alikuwa katika mishemishe za kumjibu Wema kwa kuzindua mjengo wake wa kisasa uliopo Tegeta, jijini Dar.

Akizungumza na paparazi wetu akiwa kwenye eneo ilipo nyumba hiyo ambayo ilikuwa ikifanyiwa ‘finishing’, Diamond alisema kuwa nyumba hiyo yenye thamani ya Sh. milioni 260 ni zawadi kwa mama yake Sanura Kassim ‘Sandra’.
“Mama yangu ndiyo kila kitu kwangu, mara ya kwanza nilimnunulia gari aina ya Toyota Alteeza nikaona haitoshi, nikaamua kumjengea hii nyumba ambayo itakuwa kama urithi wake hata nikifa leo,” alisema Diamond.

Diamond alimzungusha paparazi wetu na kujionea mjengo huo wenye vyumba vinne vya kulala ambavyo vyote ni ‘self contained’ (chumba chenye choo na bafu), studio kubwa ya kurekodi muziki, eneo ambalo limetengwa kwa ajili ya kujenga bwawa la kuogelea ‘swimming pool’, uwanja wa basketball na sehemu maalum ya kufanyia mazoezi (gym) ambapo alisema hadi ifikapo Septemba, mwaka huu kila kitu kitakuwa kimekamilika.

Ukiachana na ukubwa wa nyumba hiyo, uwanja ambao ameuzungushia uzio wa ukuta kuna nyumba nyingine ndogondogo tatu ambazo kwa mujibu wa staa huyo wa Songi la Kesho, zitakuwa zikipangishwa.

Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment